Search This Blog

Friday, February 10, 2012

CHADEMA WASABABISHA MAREKEBISHO YA SHERIA YA KATIBA

Tutakuwa hatutendi haki kama hatutasimama kama Watanzania kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) kwa kusimamia kidete suala la Katiba mpya mpaka sasa marekebisho ya sheria ya Katiba mpya yakapitishwa na bunge leo.Ni wazi watu mbalimbali akiwemo Rais Kikwete wamechangia hili lakini bila kumung’unya maneno niseme kama si CHADEMA kusingekuwa na hoja hii ya Katiba mpya leo.

Kwanini?

· CHADEMA iliweka suala la Katiba mpya kwenye ilani yake ya Uchaguzi mwaka 2010
· Wabunge wa CHADEMA walitoka nje ya bunge siku Rais alipolifungua bunge pamoja na mambo mengine kudai katiba mpya itakayotoa fursa ya kuwa na tume huru ya uchaguzi
· Mwaka mzima wa 2011 CHADEMA iliongoza maandamano nchi nzima kutoa elimu ya uraia na kutaka kuungwa mkono na UMMA juu ya kupata katiba mpya
· Wabunge wa CHADEMA walitoka nje ya bunge mwezi Novemba 2011 kupinga mswada wa Katiba mpya uliokuwa na Mapungufu mengi na ya kimsingi
· Kamati kuu ya CHADEMA ilinyoosha Mkono wa mapatano na serikali kwa kukutana na Rais Kikwete kupinga mswada uliokuwa mbovu uliopitishwa kiushabiki na wabubge wa CCM na CUF
· Rais aliridhia mapendeklezo yote ya CHADEMA na kuamuru mabadiliko ya sheria iliyokuwa imepitishwa kishabiki na wabubge wa CCM na CUF
· Hatimaye marekebisho ya sheria yakapitishwa na bunge na kufungua rasmi mlango wa kutengeneza katiba mpya ya Tanzania.

Ni wazi kwa yote yaliyotajwa hapo juu yanatufanya tuamini CHADEMA imesimama imara katika kupigania Katiba ya nchi.Watanzania wengi walikata tamaa na kudhani baada ya mswada mbovu kupitishwa mwaka jana CHADEMA ingesusia moja kwa moja zoezi zima.Lakini CHADEMA imejenga taswira tofauti kwa Watanzania kwa kupigana kwa hali yoyote kuhakikisha Katiba mpya inapatikana.

Wafuatao wanastahili heshima ya pekee:

Pamoja na CHADEMA kama taasisi kuonekana kukomaa na kusimamia agenda zake,ni lazima tuwatambue baadhi ya watu walioongoza mpambano huu kwa Amani na utulivu na siku moja wataingia katika vitabu vya historia
· Dr Wilbroad P. Slaa-Ni kiongozi makini,madhubuti na anayeweza kuyasimamia maneno yake kwa kuinadi ilani ya CHADEMA nchi nzima wakati wa kugombea urais mwaka 2010 na watu wakaamini na kuona umuhimu wa Katiba mpya.Lakini Pia ni Katibu mkuu ambaye ni mtendaji mkuu wa chama anayeongoza sekretariati ya chama inayopanga agenda za chama na kusimamia mikakati yote ya chama,suala la Katiba mpya likiwa mojawapo ya mkakati.
· Freeman A.Mbowe-Huyu ni kiongozi wa upinzani bungeni na muda wote ameiongoza vema kambi ya upinzani bungeni kusimamia agenda hii ya katiba mpya.Hakutetereka na amekuwa akisimamia uwajibikaji wa pamoja wa kambi yake bungeni.Kwa jinsi leo alivyohitimisha mswada huu wa katiba mpya hawezi kusahaulika kirahisi.Amewafanya watanzania sasa kutambua ni nini maana ya kambi ya upinzani bungeni.
· Zitto Z.Kabwe-Huyu ni Naibu kiongozi wa upinzani bungeni na siku zote amekuwa msaidizi muhimu na wa kuaminiwa wa kiongozi wa upinzani bungeni.Ni wazi amesaidia sana kuifanya kambi ya upinzani kuwa kama jinsi ilivyo na anastahili kufurahia matunda ya kupigania katiba mpya ndani ya bunge.
· Tundu A.Lissu-Ni mnadhimu mkuu wa upinzani bungeni.Huyu ukitaja jina lake kwa sasa hata mtoto mdogo anamjua.Hili ni jembe kweli kweli.Alipinga kwa nguvu zote mswada mbovu wa mwaka jana.Kutokana na upinzani wake kwa mswada wabunge wa CCM na CUF walimshambulia kwa kila neno baya ili kumchafua mbele ya jamii.Lakini alisimama kidete kupambana ndani na nje ya bunge mpaka leo hii walau watanzania wanafurahia mabadiliko ya sheria ile.
· Wabunge wote wa CHADEMA-Hawa kwa ujumla wao wamesimama kidete kwa umoja ndani na nje ya bunge kuhakikisha katiba mpya inapatikana.Kila walichokifanya kuhusu katiba ni msimamo wa chama chao.Wote walinena lugha moja.Hakika huu ni mfano wa kuigwa kwa vyama vingie pale kunapokuwa na jambo la msingi la kuwatetea watanzania.Iliwashangaza wengi pale hata mbunge wa Maswa John Shibuda alipoungana na wenzake mwaka jana kutoka nje ya bunge kususia mswada mbovu uliowasilishwa.
  • Rais Jakaya Kikwete-Kwa heshima ya Pekee anastahili pongezi za dhati kabisa kwa uamuzi wake wa kukubali mwito wa kukaa na CHADEMA.Ni wazi Rais alikubali kuweka pembeni itikadi ya chama chake na kuamua kuwasikiliza CHADEMA na hatimaye kuyakubali madai yao yote.Ilihitaji moyo mkuu kufanya hivi.Aliipuuza kelele za wana CCM wenzake waliokuwa hawataki akubaliane na CHADEMA.Aliwapuuza na kuwadharau wabunge wa chama chake waliotishia kupiga kura ya kutokuwa na Imani na Rais kisa eti amekubali mapendekezo ya CHADEMA ili kupata katiba bora kwa Taifa letu.Wana CCM wengine wakadiriki kusema Rais anafanya haya kwa vile anamaliza muda wake wa urais kwa hiyo anajiandalia mwisho mwema,lakini hata hawa pia Rais aliwapuuza kwa maslahi ya Katiba bora.Kwa hili hakika Jakaya Kikwete amejiandikia historia ambayo haitafutika kirahisi.
Kwa ufupi kabisa niseme waliyoyafanya CHADEMA yameingia kwenye historia mpya.Yatasimuliwa vizazi na vizazivijavyo na ni mfano kwa wanasiasa na vyama vingine vyote.Hakika wameonyesha ukomavu wa hali ya juu.Na labda niseme lakini msiniite mtabiri! Kwamba ikipatikana Katiba mpya ya watu,ambayo itatoa tume huru kabisa ya uchaguzi itakayotenda haki kwa vyama vyote mwaka 2015,basi watanzania msishangae kumuona Michael Satta wa Tanzania akimrithi Jakaya Kikwete.Na tusubiri tuone.

Mungu awatangulie watanzania katika kupata katiba bora mpya ya Tanzania.Alilolipanga Mungu mwanadamu kamwe hawezi kulipangua.

CHANZO: jamii forum: by fmpiganaji;

No comments:

Post a Comment